Monday, July 30, 2012

Na Wabunge Wetu Wengine Ni Wezi, Hakyamungu


Ndugu zangu,

Waziri Muhongo ameusema ukweli wake kule Dodoma. 
Nami nimefuatilia sinema hii ya Dodoma, kila inavyoendelea 
ndivyo ninavyozidi kuchoka. Ama hakika, tunakokwenda siko, 
tuna lazima ya kujipanga upya.

Namsifu Waziri Muhongo kwa ujasiri wake. Amutusaidia sana 
kuyajua yale ambayo yangetuchukua muda mrefu kuyajua. 
Kwa kusimama kwenye ukweli Waziri Muhungo ameitendea 
haki nchi yetu tuliyozaliwa. 

Na tulipofikia hapa ni ukweli tu ndio utakaotusaidia kutupa 
ahueni ya hali mbaya tuliyonayo kama taifa. Huu si wakati 
wa kutanguliza siasa za vyama bali kuitanguliza Nchi yetu 
tuliyozaliwa na tunayoipenda. Kutanguliza uzalendo.
Leo tunabaki vinywa wazi kusikia kuwa hata wachungaji, 
na wengine wamejiingiza Bungeni, kuwa nao wanawaibia 
Watanzania wenzao. Kwamba nao hawatosheki. Wanaiba 
huku wakitaja neno la Mungu. Leo hata wale wanaojinadi 
kuwa ni watetezi wa wanyonge wameanza kutiliwa mashaka. 
Uwezo wao wa kiuchumi unahusianishwa na ' madudu' kama 
haya ya Tanesco. Na kuna hata wenye ' kuwafuturisha' wenzao 
wenye uwezo kwa fedha walizowaibia  wananchi wanyonge.
 Hawa hawana cha swaumu bali wanashinda na njaa kwa 
dhambi ya wizi wao.


Tuna lazima sasa ya kuamka na kuwabana wezi wetu. Mwizi 
ni mwizi tu, hata kama ni mheshimiwa Mbunge.Na ukweli ndio
 unaohitajika sasa. Na si nusu ukweli, bali ukweli mzima hata 
kama  utatugharimu maisha yetu. 

Nimepata kusimulia   kisa cha kijana aliyehangaika sana 
kuusaka ukweli. Katika pitapita zake akaliona duka. Kibao 
kimeandikwa dukani ; ” Hapa tunauza ukweli”.

Dukani hapo ukweli unauzwa kwa kilo. Bei ya robo kilo 
ya ukweli imeandikwa, vivyo hivyo,bei ya nusu kilo ya ukweli.
 Lakini, mwenye duka hakuandika bei ya ukweli mzima,  
kwa maana ya kilo nzima ya ukweli.

Kijana yule akauliza; ” Mie nataka ukweli kilo nzima, mbona 
hujaandika bei?”
” Alaa,  unataka kilo nzima ya ukweli?” Aliuliza mwenye duka.
” Naam” Akajibu kijana yule.
” Basi, zunguka uje ndani nikuambie bei yake”.

Alipoingia ndani dukani, kijana yule akaambiwa;
” Kijana, hatukuandika bei, maana, gharama ya ukweli 
mzima ni uhai wako. Je, uko tayari?”

Kijana yule akatimua mbio. Nyuma aliacha vumbi. Hakuwa 
tayari kulipa gharama ya ukwelimzima.
Katika Uislamu inasemwa;  sema ukweli, hata kama unauma 
na kwamba unaweza kupelekea umauti wako.
Hakika, maandiko ya kwenye vitabu vya dini zetu hizi yana ya
kutufundisha. 

Na hilo ni Neno langu la Leo.

Maggid Mjengwa,
Sweden.

No comments:

Post a Comment