Sunday, November 25, 2012

UGANDA YAWACHINJA KENYA KATIKA UFUNGUZI WA CHALENJI CUP

WENYEJI Uganda, The Cranes wameanza vema michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Tusker Challenge baada ya kuilaza Kenya, Harambee Stars bao 1-0 kwenye Uwanja wa Mandela, uliopo Namboole, Kampala, Uganda.

Kizito akishangilia baada ya kufunga usiku huu Uwanja wa Mandela. Kushoto ni Hamisi Kiiza akimkimbilia kumpongeza

Shukrani kwake, mshambuliaji wa Saigon Xuan Thanh ya Vietnam, Geoffrey Kizito aliyefunga bao hilo pekee la ushindi dakika ya 74, akiunganisha krosi ya Iguma Dennis.

Kiungo wa Uganda, Issac Isinde akimtoka beki wa Kenya

Kwa ushindi huo, Korongo wa Kampala anafungana na Ethiopia kuongoza Kundi A, kwa pointi zake tatu kila timu.
Hadi mapumziko hakuna timu iliyofanikiwa kuona lango la mwenzake na timu zote zilishambuliana kwa zamu.
Kenya walianza kwa kasi kwa dakika tano wakicheza soka iliyowasisimua mashabiki wake wachache waliokuwapo uwanjani, lakini Uganda wakazinduka nao na kuanza kuwapa raha mashabiki wao kwa soka safi.

Mchezo uliendelea kuwa hivyo kwa timu hizo kushambuliana kwa zamu, kila upande wakicheza kwa kujiamini.Lakini sifa ziende kwa safu zote mbili za ulinzi kutokana na kucheza kwa umakini wa hali ya juu.


Kipindi cha pili timu hizo ziliporejea uwanjani, zililazimika kusimama kwa takriban dakika saba baada ya taa za uwanjani kuzimika na baada ya mafundi kutatua tatizo hilo, ndipo kabumbu likaanza tena.


Michuno hiyo itaendelea kesho kwa mechi mbili, Burundi na Somalia saa 10:00 jioni na baadaye Tanzania Bara na Sudan saa 12:00 jioni. 



VIKOSI:
Uganda; Abel Dhaira/Hamza Muwonge, Iguma Dennis, Godfrey Walusimbi,Henry kalungi, Isaac isinde, Hassan Wasswa, Geoffrey Kizito, Moses Oloya, Emmanuel Okwi, Hamisi Kiiza na Brian Umony.

Kenya; 
Duncan Ochieng, Anthony Kimani, Abdallah Juma, Jockins Atudo, David Owino, David Ochieng, Lama Salim Mohamed, Bernard Wanyama, Humphrey Mieno, Anthony ‘Muki’ Kimani/Enock Obiero na Clifton Miheso/Paul Were.

No comments:

Post a Comment