Sunday, January 5, 2014

Gwiji la soka Eusebio Afariki Dunia

Pumzika kwa amani Eusebio
GWIJI wa soka kutoka taifa la Ureno, Eusebio amefariki dunia, akiwa na umri wa miaka 71, baada ya kusumbuliwa na matatizo ya moyo kwa muda mrefu.

Eusebio alizaliwa nchini Msumbiji kama Eusebio da Silva Ferreira na anatajwa kama mmoja wa wachezaji bora zaidi kuwahi kutokea duniani.


Aliitumikia klabu ya mjini Lisbon,Benfica FC kwa miaka 22 ambapo uwezo wake wa mbio na kasi, kuutumia vyema mguu wake wa kulia na mbinu za kimpira kulimpa umaarufu sana nchini Ureno na kubatizwa jina la The Black Pearl or the Black Panther.


Wakati wa uchezaji wake alifunga mabao 733 katika mechi 745, pia alifunga mabao tisa kwenye michuano ya kombe la dunia ya mwaka 1966 na kuwa mfungaji bora wa mashindano hayo na kuisaidia Ureno kushika nafasi ya tatu kwenye michuano hiyo.
Eusebio da Silva Ferreira alikuwa mfungaji bora wa fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika nchini England mwaka 1966 kuanzia Julai 11, hadi Julai 30 wenyeji England wakiifunga Ujerumani Magharibi 4–2 na kutwaa Kombe.
Eusebio alifunga mabao tisa na kuwapiku Helmut Haller mabao sita, Geoff Hurst, Franz Beckenbauer, Ferenc Bene na Valeriy Porkujan mabao manne kila mmoja na Luis Artime na Bobby Charlton waliofunga matatu kila mmoja. 
Eusebio aliyezaliwa Januari 25, mwaka 1942, anachukuliwa kama mchezaji bora daima kuwahi kutokea duniani na Shiriksiho la Viwango la Kimataifa (IFFHS). Aliisaidia Ureno kushika nafasi ya tatu kwenye fainali hizo kwa mabao yake hayo, sita akifunga kwenye Uwanja wa Goodison Park na kuchaguliwa kuwa Mwanasoka Bora Ulaya mwaka 1965. Aliichezea Benfica kwa miaka 15 na ndiye mfungaji bora daima wa klabu hiyo.

No comments:

Post a Comment