|
Waziri
wa Kazi na Ajira, Makongoro Mahanga (kulia) akimkabidhi Ngao ya Jamii,
Nahodha wa Simba, Juma Kaseja. Pembeni yake ni beki Nassor Masoud
'Chollo' na kulia kabisa ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Shirikisho la
Soka Tanzania (TFF), Athumani Nyamlani. |
SIMBA SC,
inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager imetwaa Ngao ya Jamii, baada
ya kuifunga Azam FC, mabao 3-2 jioni hii kwenye Uwanja wa Taifa, Dar e s Salaam.
Shujaa wa Simba
leo hii alikuwa ni kiungo Mwinyi Kazimoto aliyefunga bao la ushindi dakika ya
78 kwa shuti kali la mbali baada ya kumchungulia kipa wa Azam, Deo Munishi ‘Dida’
amekaaje.
Hadi
mapumziko, Azam walikuwa mbele kwa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na John
Raphael Bocco ‘Adebayor’ na kipre Herman Tchetche, wakimtungua kipa namba moja
Tanzania, Juma Kaseja.
Bocco
alitangulia kufunga dakika ya tano ya mchezo huo, baada ya kupigiwa kona fupi
na Abdi Kassim ‘Babbi’, akatoa pasi kwa Abdulhalim Humud ambaye alimrudishia
mfungaji huyo akafumua shuti kali la chini likajaa nyavuni pembezoni mwa lango
kulia.
Bocco ambaye
alikuwa mwiba mchungu kwa safu ya ulinzi ya Simba SC leo, alimtoka Amir Maftah
upande wa kulia wa Uwanja na kuingia ndani kabla ya kutoa krosi fupi kwa Kipre
aliyemtungua Kaseja na kuipatia Azam bao la pili dakika ya 35.
Simba
ilipata bao lake la kwanza dakika ya kwanza ya muda wa nyongeza, baada ya
kutimu kwa dakika 45 za kipindi cha kwanza, mfungaji Daniel Akuffo kwa penalti,
baada ya Said Mourad kuunawa mpira kwenye eneo la hatari.
Kipindi cha
pili Simba walirudi na nguvu zaidi na kuamua kushambulia kwa mipira ya pembeni,
ikiwatumia Mrisho Ngassa na Emanuel Okwi ambao walikuwa wakibadilishana reli.
Kwa staili
hiyo, haikushangaza Simba ilipotumia dakika 45 za mwisho kwa kufunga mabao
mawili yaliyowatoa nyuma kwa 2-1 na kuibuka kidedea kwa ushindi wa 3-2.
Emanuel Okwi
alimchambua kama karanga Erasto Nyoni na kuingia ndani kabisa akiwatoka mabeki
wengine wa Azam, kabla ya kuujaza mpira nyavuni kwa shuti kali na Kazimoto akamaliza
kazi dakika ya 78.
Kwa ujumla
katika mchezo huo, Azam ilitawala kipindi cha kwanza na ilikosa mabao mawili
zaidi ya wazi kupitia kwa Himid Mao na Kipre, lakini kipindi cha pili Simba
walitawala mchezo na kama wangekuwa makini, nao wangeweza kuvuna mabao zaidi.
Naibu Waziri
wa Kazi, Makongoro Mahanga alimkabidhi ngao Nahodha wa Simba, Juma Kaseja baada
ya mechi hiyo, ambaye alikwenda kushangilia na wachezaji wenzake na mashabiki
wa timu hiyo.
Hii ni mara
ya pili mfululizo Simba wanatwaa Ngao, baada ya mwaka jana pia kuibeba
wakiifunga Yanga 2-0.
Aidha, hiyo
inakuwa mechi ya tano ya Ngao ya Jamii kuchezwa kihistoria nchini na ya pili
kuishirikisha timu nje ya wapinzani wa jadi wa soka ya Tanzania, Simba na
Yanga.
Mtibwa
ilicheza na Yanga mwaka 2009, baada ya Simba kugoma na ikashinda mabao 2-1 na
kutwaa Ngao, wakati kabla ya hapo, mwaka 2001, Ligi Kuu ya Tanzania ikiwa bado
inadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia ya Safari Lager,
ilichezwa mechi ya kwanza ya Ngao kihistoria.
Katika mechi
hiyo, Yanga ilishinda mabao 2-1 dhidi ya Simba na mwaka juzi Yanga iliifunga
tena Simba kwa penali 3-1 kufuatia sare ya 0-0 na mwaka jana, Simba ilitwaa
Ngao ya kwanza katika historia yake, kwa kuifunga Yanga mabao 2-0.
Ikumbukwe
mara ya mwisho Simba SC ilipokutana na Azam FC, katika Robo Fainali ya Klabu
Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, Julai mwaka huu, Dar es
Salaam, ilifungwa mabao 3-1, yote yakifungwa na Bocco na lile la kufutia
machozi kwa wekundu hao Msimbazi liliwekwa kimiani na kiraka Shomari
Kapombe.
Katika mchezo huo, kikosi cha Simba
kilikuwa; Juma Kaseja, Nassor Masoud
‘Chollo’, Amir Maftah, Paschal Ochieng/Juma Nyosso dk 73, Shomary Kapombe, Ramadhan
Chombo/Amri Kiemba dk69, Mrisho Ngassa, Mwinyi Kazimoto, Daniel Akuffo/Abdallah
Juma dk64, Haruna Moshi na Emanuel Okwi.
Azam FC; Deo Munishi ‘Dida’,
Ibrahim Shikanda, Erasto Nyoni, Said Mourad, Aggrey Morris, Abdulhalim Humud,
Ibrahim Mwaipopo/Salum Abubakar dk 58, Himid Mao, John Bocco, Abdi Kassim/Kipre
Michael Balou dk 69 na Kipre Herman Tchetche/Zahor Pazi dk 82.
|
11 wa Simba walioanza leo |
|
11 wa Azam walioanza leo |
|
Bao la kwanza la Azam |
|
Bao la kwanza la Azam |
|
Azam wanashangilia bao la kwanza |
|
Hatari kwenye lango la Simba |
|
Hatari kwa kwenye lango la Simba, Kaseja chini kule |
|
Himid Mao alikaribia kufunga baada ya kumvisha kanzu Kaseja, lakini mpira ukapaa juu kidogo |
|
Kipre Tchetche akiwatoka mabeki wa Simba |
|
Azam wanashambulia |
|
Hatari kwenye lango la Simba |
|
John Bocco anamtoka Maftah |
|
Bocco anatoa pasi ya bao |
|
Humud anampongeza Bocco kufunga |
|
Bocco anampongeza Kipre kuitumia vema pasi yake |
|
Mashabiki nwa Simba |
|
Akuffo akiwa amembeba Okwi baada ya kufunga bao la kusawazisha |
|
Abdallah Juma akumpongeza Kazimoto kufunga la ushindi, Anyeipa mgongo kamera ni Nyosso |
|
Kazimoto akiwapungukia mkono mashabiki wa Yanga baada ya kufunga la ushindi. Kulia Nyosso na kushoto Abdallah Juma |
|
Mashabiki wa Simba wakiwa na jezi iliyoandikwa Kagawa Ngassa |
|
Kushoto Kaseja, kulia Ngassa na Akuffo wakicheza kiduku |
|
Ngassa akishangilia kwa staili ya aina yake |
|
Nyamlani akimpa mkono wa pongezi Akuffo. Anayemfuatia ni Waziri Mahanga, akiwasubiri Ngassa na Komabil Keita |
No comments:
Post a Comment