Thursday, January 17, 2013

Watanzania 80,000 kupata ajira Mradi wa Mabasi yaendayo kasi

BODI ya Wakurugenzi ya Benki ya Dunia (WB), imeidhinisha Dola za Marekani 100 milioni kwa ajili ya Mradi wa Mabasi yaendayo Kasi (BRT) jijini Dar es Salaam.

Taarifa ya benki hiyo iliyopatikana Dar es Salaam jana imeeleza kuwa mradi huo utakaozalisha ajira 80,000 kwa Watanzania, utasaidia abiria 300,000.

“Ajira hizo 80,000 zitapatikana hadi mwaka 2015 na zitatokana na kazi zinazotarajiwa kuwapo, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa barabara, vituo vya abiria, vituo vidogo na vituo vya kuratibu barabara hiyo,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, Philippe Dongier alisema kiasi hicho cha fedha kimelenga kukamilisha awamu ya pili ya mradi huo.


Dongier ambaye pia ni msimamizi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Uganda na Burundi, alisema mradi huo utagharimu jumla ya Dola za Marekani 290 milioni.

“Dar es Salaam inakuwa kwa kasi, msongamano wa magari ni tatizo kwa ukuaji wa uchumi kwa sababu unapunguza uzalishaji kwa kupoteza muda wa watumiaji wa barabara. Hali hiyo inatishia ukuaji wa baadaye wa mji na nchi kwa jumla na unaongeza uharibifu wa mazingira,” ilisema taarifa ya WB na kuongeza:

“Mfumo wa BRT utasimamiwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi kwa Dola za Marekani 40.9 milioni ukihusisha wasimamizi binafsi wawili wa mabasi na mkusanya nauli mmoja. Mfumo huo mpya utatekelezwa kwa mabasi yapatayo 148 yatakayokuwa na uwezo wa kubeba abiria 140 kila moja kwa safari za haraka na za kawaida.


“Mabasi mengine 100 yenye uwezo wa kubeba abiria 60 kila moja yatatembea katika barabara ndogo. Kutakuwa na kilometa 20.9 zitakazokuwa na njia za waendesha baiskeli na wapita kwa miguu kila upande na vituo vya mabasi kwa kila umbali wa wastani wa mita 500.”

Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka alisema hana taarifa za benki hiyo kuidhinisha fedha hizo, lakini akasema atafuatilia ili kujua idadi ya ajira, hasa zitakazowanufaisha wazawa.

“Kwa kweli hizo taarifa ndiyo kwanza nazisikia kwako, labda unipe muda nizifuatilie ili nije na majibu ya uhakika. Lakini kama kawaida, ajira za kampuni kama hizo huwa na wataalamu wa nje na wa ndani, kwa hiyo tutahakikisha kuwa sheria zinalindwa,” alisema Kabaka.

Mtaalamu wa usafiri katika Benki ya Dunia, Yonas Mchomvu alisema: “Tunafurahishwa na kasi ya utekelezwaji wa mradi wa mabasi yaendayo kasi, hasa kwa kuwa makandarasi wote wanaotakiwa wameshapewa fedha na ujenzi unaendelea,” alisema Mchomvu.

Daladala wachekelea

Licha ya taarifa hiyo kueleza kuwa mradi huo utasababisha kuondolewa kwenye mzunguko daladala 1,800, bado wamiliki wa magari hayo wamepokea mradi huo kwa furaha.
Mwenyekiti wa Wamiliki wa Daladala Dar es Salaam (Darcoboa), Sabri Mabrouk alisema hiyo ni fursa kubwa kwao ambayo hawako tayari kuikosa.

“Siyo kwamba mradi huo utatuathiri na siyo daladala 1,800 tu zitakazoondolewa, ni daladala 3,000. Sisi ndiyo walengwa wa mafanikio hayo kwani hayo mabasi yanayokwenda haraka tutamilikishwa. Hapa ndipo tunahimizana kujiunga ili tujue tutayamiliki vipi,” alisema Mabrouk.


Mabrouk alisema daladala zitakazoondolewa kwenye mzunguko zitahamishiwa kwenye barabara nyingine, hivyo akaitaka Sumatra kutosajili daladala nyingine wakati mradi huo utakapoanza kazi.

“Mradi huu siyo kwamba utaishia Barabara ya Morogoro tu, utakwenda pia Barabara ya Kilwa na baadaye Barabara ya Nyerere na nyinginezo. Mwenzako akinyolewa wewe nywele zako tia maji. Kwa hiyo kila mmiliki wa daladala atafaidika, cha msingi tujiweke tayari kwani tukiipoteza nafasi hii itachukuliwa na watu wengine,” alisema Mabrouk.

Mkandarasi wa mradi
Meneja wa mradi huo kutoka Kampuni ya Ujenzi ya Strabag ya Ujerumani inayojenga barabara hiyo, Frank Rohde alisema mradi umegawanyika katika vipindi tofauti.
Alisema awamu ya kwanza itakuwa ni maendeleo ya barabara kutoka Magomeni hadi Kimara ambayo itajengwa vituo 15 vya mabasi... “Katika awamu hii, vituo vikuu viwili vitajengwa ambavyo ni Kimara na Ubungo.”

Anasema awamu ya pili itajumuisha uboreshaji wa barabara kutoka Magomeni, Kivukoni, Barabara ya Kawawa kutoka Magomeni hadi Morocco na Barabara ya Msimbazi kutoka eneo la Faya hadi Kamata kupitia Kariakoo.
“Katika maeneo hayo yote, kutajengwa vituo 14 vya mabasi hadi Kituo cha Morocco,” alisema.

Rohde alisema ujenzi wa barabara za mabasi hayo utajumuisha barabara za mabasi ya kawaida ya umma na zitapanuliwa ili kuwekwa njia mbili zaidi kwa waenda kwa miguu na waendesha baiskeli.
“Vituo vitajengwa katikati ya barabara hizo (za mabasi ya kasi) katika kila mita 500-700 na vituo vikuu ni vitano,” alisema.

Mradi huo umefadhiliwa na Benki ya Dunia, mwajiri mkuu akiwa ni Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), washauri wa ujenzi ni Kampuni ya SMEC kutoka Australia.
Kutakuwa na huduma za haraka safari za kutoka Kimara Mwisho hadi Posta Mpya zitakazochukua dakika 25 na kwa huduma za kawaida safari zitachukua dakika 30 hadi 40.

Shughuli nyingine zitakazofanywa katika mradi huo ni pamoja na kutengeneza mabomba ya maji ya kunywa, kuimarisha mitandao ya simu, taa za barabarani na za kuongozea magari.
Mradi huo ulioanza Februari, 2012 utachukua miaka mitatu kukamilika. Kilomita 17 za awali zinatarajiwa kumalizika katika kipindi cha miaka miwili.

Kuhusu ajira, Ofisa Habari wa SMEC, Amina Juma alisema Strabag na SMEC walitafuta vijana wenye taaluma kwa ajili ya kufanya kazi katika mradi huo, akisema kampuni yake ilihakikisha kuwa wanaopata ajira zaidi ni wazawa ambao wanaielewa nchi yao.

No comments:

Post a Comment