Wednesday, June 1, 2016

TAARIFA KWA WANAJUMUIYA WA TANZANIA HOUSTON COMMUNITY (THC) NA UMMA KWA UJUMLA

Uongozi wa Tanzania Houston Community (THC) unapenda kukanusha taarifa zisizo sahihi zinazosambazwa mitandaoni ya kwamba ubalozi wa Tanzania nchini Marekani chini ya Mh. Balozi Wilson Masilingi haukufanya lolote wakati jumuiya yetu ilipopatwa na misiba miwili ya Bw.Henry Kiherile na Bw.Andrew Nicky Sanga iliyotokea kwa nyakati tofauti mapema mwezi April mwaka huu.

Uongozi  wa THC unapenda umma utambue kwamba tulipata na tunathamini sana ushirikiano ulioonyeshwa na kutolewa na ubalozi pamoja na balozi mwenyewe Mh. Masilingi wakati wa misiba hiyo miwili na hata baada ya shughuli hizo za misiba kumalizika.

Marehemu Andrew Sanga ( kushoto ) na Marehemu Henry Kiherile ( kulia ) enzi za uhai wao
Baadhi ya mambo yaliyofanywa na balozi ni kuwatafuta viongozi wa jumuiya THC na kuzungumza nao mapema baada ya misiba hiyo kutokea (balozi alitutafuta viongozi na si vinginevyo) ambapo alizungumza na Rais wa jumuiya Bw. Daudi Mayocha kwa simu na Katibu mkuu wa  jumuiya Bw. Michael Ndejembi na kuwapa pole kwa niaba ya familia na jumuia nzima.

Uongozi unafahamu kwamba sababu za balozi kushindwa kufika Houston wakati wa misiba hiyo ni yeye kumuwakilisha Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Magufuli kwenye kongamano la DICOTA lililokuwa likifanyika jijini Dallas, Texas. Tunatambua pia kwamba nia ya balozi kuja Houston bado iko pale pale.

Aidha Balozi Masilingi alimtuma afisa ubalozi Bw. Dismas Assenga kumuwakilisha katika shughuli za Misa na Kuaga mwili wa marehemu Andrew Nicky Sanga, ambapo afisa huyo pamoja na mambo mengine alitoa salamu za rambirambi toka kwa balozi na alikabidhi rambirambi ya $500 kwa kila familia pamoja na  kuzungumza na wafiwa hao kwa nyakati tofauti.

Kwa taratibu za kiupelelezi Uongozi wa THC hauwezi kutoa taarifa zaidi ya namna suala hili linavyoshughulikiwa kati ya vyombo vya usalama nikimaanisha HPD Homicide Department na Ubalozi wa Tanzania lakini tunatambua kwamba ubalozi unafuatilia kesi zote mbili kwa ukaribu sana.

Uongozi wa THC unasisitiza kuwa hauhusiki kwa aina yoyote na Waraka (Petition) unaosambazwa kwenye mitandao kumchafua Balozi Masilingi na ubalozi wetu wa Washington D.C kwa ujumla.


Daudi Mayocha,
Rais wa Jumuiya ya Watanzania Houston (THC)

thc.leaders@gmail.com

No comments:

Post a Comment